Tume ya Kitaifa ya Haki za Kibinadamu ya Kenya (KNCHR) imetangaza kuwa idadi ya watu waliouawa katika maandamano ya Sabasaba yaliyofanyika hivi karibuni nchini humo imefikia 31.
Idadi hiyo ni mara mbili ya ile iliyotangazwa awali na Polisi wa Kenya.
Katika taarifa iliyotolewa siku ya Jumanne, KNCHR ilisema kuwa zaidi ya watu 107 walijeruhiwa, na takriban 532 walikamatwa wakati wa maandamano hayo.
Pia imeripotiwa kuwa watu wawili hawajulikani waliko.
Tume hiyo pia ilitaja kuwa kuna uharibifu mkubwa wa mali, ingawa thamani kamili bado haijabainishwa.
Rais wa KNCHR, Raymond Nyeris, alisema kuwa wote waliohusika, iwe ni raia au polisi, wanapaswa kuwajibika kwa matendo yao.
Alisema:
“Tunalaani vikali ukiukaji wote wa haki za kibinadamu na tunataka wahusika wote wawajibishwe.”
Maandamano ya Sabasaba yalifanyika tarehe 7 Julai, kwa ajili ya kuadhimisha miaka 35 tangu Wakenya walipomtaka Rais wa wakati huo, Daniel Arap Moi, kuanzisha mfumo wa vyama vingi vya siasa.
Maandamano hayo yaliambatana na vurugu kali kati ya raia na polisi, zikitumika vifaa vya machozi, mawe, na risasi za moto.


