Rais wa Marekani, Donald Trump, ametangaza kuwa baadhi ya wafanyakazi wa Marekani wameondolewa katika Mashariki ya Kati kutokana na mazungumzo ya silaha za nyuklia na Iran ambayo huenda yasifanikiwe na kuhatarisha maisha yao.
Alipoulizwa kuhusu taarifa hizo za kuondolewa kwa wafanyakazi, Trump aliwaambia waandishi wa habari mjini Washington:
“Ni kweli wanaondolewa kwa sababu eneo hilo linaweza kuwa hatari.”
“Tulitangaza onyo la kuondoka, tutaona hali itakavyokuwa.”
Alipoulizwa jinsi mvutano katika eneo hilo unaweza kupunguzwa, Trump alisema:
“Hawawezi kumiliki silaha za nyuklia, hilo ni jambo rahisi sana. Hatutaruhusu hilo kutokea.”
Kwa mujibu wa taarifa, Ubalozi wa Marekani nchini Iraq ulikuwa ukijiandaa kwa kuondoa baadhi ya wafanyakazi, huku ruhusa ya kuondoka kwa hiari ilitolewa Bahrain na Kuwait.
Mnamo Jumatano, Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani ilisasisha tahadhari zake za safari kwa raia wake duniani kote ili kuonyesha hali ya sasa.
Taarifa iliyotolewa ilisomeka:
“Tarehe 11 Juni, Wizara ya Mambo ya Nje iliamuru kuondoka kwa wafanyakazi wasio wa lazima wa serikali ya Marekani kutokana na hali ya wasiwasi katika eneo hilo.”
Trump amekuwa akitoa vitisho vya kuivamia Iran endapo mazungumzo kuhusu mpango wa nyuklia wa nchi hiyo hayataendelea vizuri, kama ilivyoripotiwa na Deutsche Welle.
Mnamo Jumatano, Rais wa Marekani alisema kuwa anazidi kupoteza matumaini kuwa Tehran itakubali kusitisha urutubishaji wa uranium — jambo ambalo ni hitaji kuu la Marekani.
Aidha Jumatano hiyo hiyo, Waziri wa Ulinzi wa Iran, Aziz Nasirzadeh, alitangaza kuwa iwapo Iran itashambuliwa, itajibu kwa kulenga kambi za kijeshi za Marekani katika eneo hilo.
Kwa sasa, Marekani ina kambi za kijeshi nchini Iraq, Kuwait, Bahrain, Qatar, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), na maeneo mengine.


