Serikali ya Rwanda imesaini mkataba wa kushirikiana na klabu ya Atlético de Madrid kutoka Hispania kwa ajili ya kutangaza utalii wa Rwanda kupitia chapa ya ‘Visit Rwanda’. Mkataba huu umesainiwa na Bodi ya Maendeleo ya Rwanda (RDB) na utadumu hadi Juni 2028.
Kupitia mkataba huu, maandishi ya ‘Visit Rwanda’ yataonekana kwenye sare za mazoezi za wachezaji wa Atlético Madrid pamoja na zile wanazovaa wakati wa kupasha moto kabla ya mechi. Hii itaanza kutekelezwa katika mechi tano za mwisho za ligi ya Hispania msimu huu na kwenye Kombe la Dunia la Klabu litakalofanyika Marekani majira ya joto mwaka huu.
Kuanzia msimu ujao, maandishi haya pia yataonekana kwenye sare za timu ya wanawake na wanaume wakati wa mazoezi, kupasha moto na pia nyuma ya jezi za mechi. Aidha, yataonekana uwanjani kwenye uwanja wa klabu hiyo wa Riyadh Air Metropolitano, kwenye mitandao yao ya kijamii na katika kampeni mbalimbali kwa mashabiki.

Mkataba huu pia unampa Rwanda nafasi ya kuwa mshirika mkuu wa Atlético Madrid katika shughuli za mazoezi na kuwa balozi rasmi wa utalii. Rwanda pia itakuwa na haki ya kipekee ya kutangaza kahawa yake kupitia klabu hiyo.
Mkurugenzi Mkuu wa Operesheni wa Atlético Madrid, Óscar Mayo, amesema kuwa ‘Visit Rwanda’ ni mshirika mzuri katika kupanua wigo wa kimataifa wa klabu hiyo, na kuitaja Rwanda kuwa nchi inayopiga hatua kubwa za maendeleo.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa RDB, Jean-Guy Afrika, amesema kuwa ushirikiano huu unalenga kuitangaza Rwanda kama kitovu cha utalii, uwekezaji na maendeleo ya michezo, na pia kutoa fursa kwa vijana wa Kiafrika kupitia kandanda.

Atlético Madrid sasa inakuwa klabu ya hivi karibuni barani Ulaya kushirikiana na ‘Visit Rwanda’, ikifuata nyayo za Arsenal (Uingereza), Paris Saint-Germain (Ufaransa) na Bayern Munich (Ujerumani).


