Baraza la Mawaziri lililofanyika Jumatano tarehe 16 Julai chini ya uenyekiti wa Rais Paul Kagame, limeidhinisha muswada wa sheria wa kuridhia rasmi mkataba wa amani uliofikiwa hivi karibuni kati ya Rwanda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
Mnamo tarehe 27 Juni, Waziri wa Mambo ya Nje wa Rwanda, Balozi Olivier Nduhungirehe, na mwenzake wa DRC, Thérèse Wagner Kayikwamba, walitia saini mkataba huo.
Mkataba huo ulifikiwa kwa usuluhishi wa Marekani.
Taarifa ya maamuzi ya Baraza hilo, iliyosainiwa na Waziri Mkuu Dkt. Edouard Ngirente, inataja mkataba huo kuwa “hatua muhimu katika kutatua matatizo ya usalama ambayo Rwanda imekuwa ikiyasisitiza, kurejesha amani na utulivu katika eneo la Maziwa Makuu, na kuimarisha ushirikiano wa maendeleo ya kanda.”
Miongoni mwa vipengele vikuu vya mkataba huo ni kwamba Rwanda na DRC zinapaswa kuheshimu mamlaka ya kila upande na kuepuka kushirikiana na makundi yenye silaha yanayokusudia kuvuruga usalama wa nchi nyingine.
Mkataba huu hasa unaitaka DRC kuvunjilia mbali kundi la kijeshi la FDLR linalohusishwa na mauaji ya kimbari, na Rwanda nayo itaondoa hatua za kiulinzi ilizoweka.
Pia unaitaka Kinshasa kufanya mazungumzo huko Doha, Qatar, na kundi la waasi la AFC/M23 linalopinga serikali yake, kwa lengo la kumaliza mgogoro uliopo kati ya pande hizo mbili.
Baraza la Mawaziri limesisitiza kuwa Rwanda imejitolea kutekeleza mkataba huo, na inasubiri matokeo ya mazungumzo ya Doha kati ya Kinshasa na AFC/M23.
Mazungumzo hayo kwa sasa yanaendeshwa na Qatar kwa kushirikiana na Umoja wa Afrika (AU).


