Katika ujumbe wa kushangaza uliovuma mitandaoni, mtumiaji wa X (zamani Twitter) anayeitwa Nibisazi aliomba Polisi wa Rwanda kumpeleka katika Kituo cha Marekebisho cha Iwawa, akisema maisha ya uraiani ni magumu sana na anatamani kujifunza fani ya kazi.
Nibisazi aliandika:
“Habari Polisi, maisha huku nje ni magumu, naomba mnichukue kunipeleka Iwawa nijifunze kazi ya mikono.”
Polisi walijibu haraka kupitia akaunti yao rasmi ya X, wakimshauri:
“Vipi kama ukaomba kujiunga na shule ya TVET ukajiajiri mwenyewe? Huenda kesho au keshokutwa ukawa wewe ndiye unatoa ajira kwa wengine, hakuna ajuaye.”
Walimshauri achague kwenda kusoma katika shule za mafunzo ya ufundi stadi (TVET), ambapo mtu yeyote anaweza kujifunza kazi anayopenda, badala ya kutegemea kituo cha Iwawa ambacho kiliundwa kusaidia watu walioko kwenye matatizo makubwa ya kitabia na maisha.
Kituo cha Marekebisho na Mafunzo ya Ufundi cha Iwawa, kilichopo katika Wilaya ya Rutsiro, kinatoa mafunzo ya ushonaji, useremala, kilimo, ujenzi, na mengineyo. Pia hutoa masomo ya kusoma na kuandika kwa wasiojua na huduma za afya ya akili.


