Vita ya Ndani Wakiso: Wanajeshi 13 wa Uganda Wakamatwa kwa Kuwapiga Polisi

Sangiza iyi nkuru

Jeshi la Polisi la Uganda limetangaza kuwa kwa kushirikiana na jeshi la nchi hiyo, wamewakamata wanajeshi 13 waliovamia kituo cha polisi katika wilaya ya Wakiso, na kuwapiga maafisa wa polisi wakiwemo kiongozi wao.

Tukio hilo lilitokea Jumatatu, tarehe 2 Mei.

Katika taarifa ya polisi, ilielezwa kuwa chanzo cha mapigano kati ya wanajeshi na polisi, ambayo yalihusisha kurushiana risasi, kilikuwa ni jaribio la wanajeshi kuwaondoa wakazi waliokuwa karibu na kituo hicho cha polisi kwa njia isiyo halali.

Wanajeshi hao ni sehemu ya kikosi kazi maalum kilichoundwa na Rais Yoweri Kaguta Museveni kwa ajili ya usimamizi wa ardhi na uhifadhi wa mazingira.

Walipofika Wakiso, waliomba msaada kwa Kamanda wa Polisi wa Wilaya (DPC) na wenzake kuwasaidia kuwaondoa wakazi hao. Hata hivyo, DPC alikataa, akisema hawakuwa na amri ya mahakama.

Taarifa ilisema:

“DPC alikataa kwa sababu hakukuwa na uamuzi wa mahakama… Kukataa kwake kuliwakera wanajeshi waliokuwa na silaha, wakaanza kumpiga. Polisi wengine waliokuwapo kituoni walijibu kwa kutumia silaha, na hali hiyo ilisababisha kurushiana risasi hadi wanajeshi wakakimbia.”

Polisi ilisema kuwa maafisa kutoka Makao Makuu ya Polisi Kampala, kwa kushirikiana na Jeshi la Wananchi la Uganda (UPDF), waliwatafuta na kuwakama wanajeshi hao huko Yesu Amala, Wakiso.

Wanajeshi hao 13 sasa wako kizuizini na watakabiliwa na adhabu za kinidhamu.

Si mara ya kwanza wanajeshi wa UPDF kuvamia vituo vya polisi. Mwishoni mwa Aprili, wanajeshi wa kikosi maalum cha SFC walivamia kituo cha polisi cha Lubowa kilichopo Kajjansi, wakawapiga polisi waliokuwemo na kuwapokonya silaha zao.

Soma Izindi Nkuru

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *