Mwanajeshi wa Uingereza aliyekuwa katika Kituo cha Mafunzo ya Jeshi la Uingereza nchini Kenya (BATUK) kilichoko Nanyuki, amekamatwa kwa tuhuma za kubaka karibu na kambi ya kijeshi.
Tukio hilo linadaiwa kutokea mwezi uliopita wakati kundi la wanajeshi wa Kiingereza walipozuru baa moja mjini Nanyuki.
Mmoja wa wanajeshi hao anashutumiwa kumbaka mwanamke wa Kenya baada ya kuondoka katika eneo hilo, kwa mujibu wa taarifa kutoka tovuti ya Kenyans.co.ke.
Kukamatwa kwake kunajiri wakati kesi nyingi zinazohusisha wanajeshi wa Uingereza wanaodaiwa kuwahodhi wanawake wa Kenya kingono zikiendelea, huku kukiwa na wito wa kuwepo kwa mfumo madhubuti wa haki na uwajibikaji.
Taarifa zinasema kuwa polisi tayari wamehoji mshukiwa, na uchunguzi bado unaendelea. Wakati huohuo, Wizara ya Ulinzi ya Uingereza imesema kuwa imeshika hatamu za kushughulikia suala hili.
Msemaji wa wizara hiyo alithibitisha kukamatwa kwa mshukiwa na kusema: “Tunaweza kuthibitisha kuwa mtu anayehudumu nchini Kenya amekamatwa.”
Msemaji huyo aliongeza: “Tabia zisizokubalika na za vurugu hazina nafasi katika jeshi letu. Taarifa yoyote ya uhalifu mkubwa inayomhusisha mwanajeshi huchunguzwa kwa uhuru…”
Alikataa kutoa maelezo zaidi, akisema kuwa uchunguzi bado unaendelea chini ya kitengo maalum cha uhalifu katika jeshi.
Tukio hili linatokea wakati nchi bado inasubiri matokeo ya uchunguzi kuhusu mauaji ya mwanariadha wa Kenya, Agnes Wanjiru, ambaye inadaiwa aliuawa na mwanajeshi wa Uingereza mwaka 2012.


