APR FC imetwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Rwanda 2024/2025, baada ya kuifunga Muhazi United kwa bao 1-0.
Muhazi United iliikaribisha timu ya majeshi ya APR FC katika Uwanja wa Ngoma, kwenye mechi ya siku ya 29 ya ligi.
Goli pekee la ushindi lilifungwa dakika ya 35 na Cheikh Djibril Ouattara kutoka Burkina Faso, baada ya kupokea pasi safi kutoka kwa Ruboneka Jean Bosco. Bao hilo lilitosha kuipatia APR FC pointi tatu muhimu kule Kibungo.
Pointi hizo ziliihakikishia APR FC taji lake la 23 katika historia ya klabu, na la sita mfululizo tangu ilipoanza kutawala ligi.
Wameibuka mabingwa baada ya wapinzani wao wakuu Rayon Sports kushindwa kupata ushindi dhidi ya Vision FC, wakiambulia sare ya 0-0.
APR FC bado inasubiri kumenyana na Musanze FC katika mechi ya mwisho. Kwa sasa inaongoza ligi kwa alama 64, ikiwa na alama nne mbele ya Rayon Sports, ambayo inakabiliwa na mechi dhidi ya Gorilla FC.


