China imetangaza ongezeko la 34% la ushuru kwa bidhaa zinazotoka Marekani, kama njia ya kujilipiza kisasi.
Uamuzi huu ulifanywa na Beijing baada ya Rais wa Marekani Donald Trump kuweka ongezeko la ushuru la 34% kwa bidhaa za China Jumatano, ambayo iliongezwa kwa ushuru wa 20% uliokuwepo, hivyo kuufanya jumla kuwa 54%.
Ijumaa, Wizara ya Fedha ya China ilitangaza kuwa ushuru huu mpya utaanza kutumika kuanzia tarehe 10 Aprili.
Wizara ilieleza kuwa uamuzi huu ulifanywa ili “kulinda usalama na maslahi ya taifa, na pia kutimiza majukumu ya kimataifa, ikiwa ni pamoja na kuepuka kuongeza gharama.”
China tayari ilikuwa imeweka ushuru wa 67% kwa bidhaa kutoka Marekani, ikimaanisha kuwa ushuru mpya unaufanya jumla kuwa 101%.
Ijumaa, Rais Donald Trump alikosoa China kupitia jukwaa lake la Truth Social, akisema kuwa China ilikuwa “imepoteza mwelekeo” na “imepoteza udhibiti.”
Mbali na kuongeza ushuru kwa bidhaa za Marekani, Beijing pia imetangaza kuwa imeandika rasmi kwa Shirika la Biashara la Kimataifa (WTO) kupinga uamuzi uliofanywa hivi karibuni na Rais Donald Trump.


