Jeshi la Ulinzi la Uganda (UPDF) limeunda kamati ya uchunguzi ya juu kuchunguza madai mapya kuhusu vitisho vya ugaidi vilivyoripotiwa mjini Kampala. Inadaiwa kuwa baadhi ya maafisa wa usalama wanaohusika na kupambana na ugaidi walivumbua matukio hayo ili wapate fedha zaidi.
Kamati hiyo inaongozwa na Luteni Jenerali Sam Okiding, Naibu Mkuu wa Majeshi, ikijumuisha viongozi waandamizi wa usalama kutoka idara mbalimbali nchini Uganda.
Miongoni mwa wanakamati ni Mkuu wa Polisi (IGP) Abbas Byakagaba; Arthur Mugyenyi, Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Usalama wa Ndani (ISO); Balozi Joseph Ocwet, Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Usalama wa Nje (ESO); Meja Jenerali Christopher Ddamulira, Mkuu wa Upelelezi wa Jinai; Brigedia Jenerali Tom Magambo, Mkuu wa Idara ya CID; na Kanali Ddamulira Sseruyange, Mkuu wa Kikosi Maalum (SFC) anayesimamia usalama wa ndani na wa kijasusi.
Vyanzo vya usalama vinasema uchunguzi huo umetokana na wasiwasi unaoongezeka katika uongozi wa juu wa jeshi na polisi kufuatia ripoti zinazokinzana kuhusu mashambulizi ya mabomu yanayodaiwa kufanywa na kundi la kigaidi la ADF linaloshirikiana na Dola ya Kiislamu kutoka mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).
Uchunguzi wa awali unaonyesha kuwa baadhi ya maafisa huenda walizua au wakazidisha matukio ili waonyeshe haja ya kuongezewa bajeti na kufikia fedha za kupambana na ugaidi.
Afisa mmoja mwandamizi wa jeshi aliye karibu na suala hilo alisema:
“Japokuwa ADF bado ni tishio, hatuwezi kuruhusu mifumo yetu ya ndani kuchezewa kwa maslahi binafsi.”
Akaongeza:
“Uadilifu wa vyombo vyetu vya usalama ni jambo la kipaumbele.”
Kwa mujibu wa ChimpReports, kamati hiyo itachambua taarifa za kiutendaji, mawasiliano ya simu, matumizi ya fedha na taarifa za kijasusi kuhusu vitisho vya mabomu kwa kipindi cha miezi sita iliyopita.
Viongozi wa juu wa polisi na ujasusi wa kijeshi pia watahojiwa.
Kamati hii imeanzishwa wakati wananchi wengi wakihoji usalama wa maeneo ya Kampala kufuatia mashambulizi yaliyodaiwa kuzuiliwa.
Msemaji wa UPDF hakupatikana kutoa maoni wakati taarifa hii ilichapishwa, lakini vyanzo vinaeleza kuwa kamati imeanza kufanya mahojiano katika makao makuu ya jeshi Mbuya.
Matokeo ya uchunguzi huo yatapelekwa kwa Mkuu wa Majeshi, Jenerali Muhoozi Kainerugaba, ambaye anadaiwa kuamuru uchunguzi huo baada ya ukaguzi wa ndani kubaini kasoro.
Uchunguzi huu ni miongoni mwa hatua kali zaidi za ndani za kupambana na ugaidi nchini Uganda katika miaka ya hivi karibuni, na unaweza kusababisha adhabu kali endapo makosa yataonekana kuwa ya kweli.


