Jumanne, Mei 13, 2025, mwigizaji maarufu wa filamu wa Ufaransa Gerard Depardieu alipatikana na hatia na mahakama ya Paris kwa kuwanyanyasa kingono wanawake wawili wakati wa utengenezaji wa filamu “Les Volets Verts” (“The Green Shutters”) mnamo mwaka 2021.
Depardieu, mwenye umri wa miaka 76, alihukumiwa kifungo cha miezi 18 kilichosimamishwa. Hakuhudhuria mahakamani kusikiliza hukumu hiyo ikisomwa.
Alishtakiwa kwa nini?
Wakati wa kesi ya siku nne mwezi Machi, wakili wake Jeremie Assous alisema mashtaka hayo yalikuwa ya kubuniwa na kuomba yafutiliwe mbali.
Mwendesha mashtaka alieleza kuwa mlalamikaji mmoja, aliyekuwa msimamizi wa mavazi kwenye seti, aliwaambia wachunguzi kuwa alisikia maneno machafu kutoka kwa Depardieu. Baadaye, alisema alinyanyaswa kimwili na Depardieu alipokuwa akiondoka setini: alimshika kwa nguvu kwenye miguu, akamgusa kiunoni, tumboni, na kifuani, huku akisema maneno ya aibu.

Mlalamikaji wa pili, msaidizi wa seti, alidai Depardieu alimshika makalio na matiti mara tatu tofauti wakati wa utengenezaji wa filamu hiyo.
Depardieu alikana mashitaka hayo lakini alikiri kutumia lugha isiyofaa na kumshika msimamizi wa mavazi kiunoni wakati walikuwa wakibishana. Alikanusha kwamba alikuwa na nia ya kimapenzi.
Kwa mujibu wa shirika la habari la Reuters, jaji Thierry Donard alisema maelezo ya utetezi ya Depardieu hayakuwa na mashiko.


