Siku nane baada ya kuuawa kwa raia sita katika wilaya ya Nyabiraba na Imbonerakure (vijana wa chama tawala CNDD-FDD nchini Burundi), mahakama ya Bujumbura ilitoa hukumu Jumanne tarehe 8 Julai.
Kesi hiyo ilisikilizwa Jumatatu na ilihitimishwa kwa adhabu kali kwa washitakiwa. Mahakama iliwagawanya walioshtakiwa katika makundi matatu. Kundi la kwanza lilijumuisha wale waliotuhumiwa kupanga na kutekeleza mauaji hayo.
Waliomo kwenye kundi hilo ni:
-
Aloys Hakizimana
-
Alexandre Ndikumana
-
Innocent Ndayisenga
-
Félix Ntirandekura
-
Kennedy Manirampa
-
Innocent Ntirampeba
-
Jean-Pascal Nahishakiye
-
Daniel Nyandwi
-
Elysée Ndayikengurukiye
-
Samuel Ndihokubwayo
Watu hawa kumi walihukumiwa kifungo cha maisha jela na kuamriwa kulipa milioni 150 za faranga za Burundi kwa familia za waathirika kama fidia.
Zaidi ya hayo, saba wa kwanza kwenye orodha hiyo waliamriwa kulipa milioni 10 zaidi, kwa mujibu wa ripoti ya RPA.
Kundi la pili lilikuwa na watu wawili waliopatikana na hatia ya ushirika katika uhalifu:
-
Aline Kwizera
-
Egide Ndayishimishe
Wote wawili walihukumiwa kifungo cha miaka 20 na faini ya milioni 15 za faranga za Burundi.
Kundi la tatu lilikuwa la viongozi wa mitaa waliotuhumiwa kwa kushindwa kusaidia watu waliokuwa hatarini. Hawa ni:
-
Meschack Nduwimana
-
Rémégie Ndikumana
-
Georges Nahimana
-
Eddy Ndihokubwayo
Kila mmoja alihukumiwa kifungo cha miaka mitatu.
Mwanzoni, watu ishirini walifunguliwa mashtaka, lakini ni watu kumi na sita pekee ndio walihukumiwa.
Wafuatao walikutwa hawana hatia:
-
Moise Bigiruwuhiriwe
-
Léonce Mpitabavuma
-
Eric Nduwimana
-
Ferdinand Ntahomvukiye
Wakati wa kesi, mwendesha mashtaka alisisitiza kuwa uhalifu huo ulikuwa umepangwa mapema, na akatoa ushahidi wa orodha ya watu waliolengwa ambayo ilikuwa imebandikwa kwenye ofisi ya PAEEJ (mpango wa serikali wa ajira kwa vijana) kabla ya mauaji hayo kutokea.


