Rais wa Rwanda, Paul Kagame, ni miongoni mwa viongozi sita wa nchi za Afrika — wakiwemo wale wa Senegal, Ghana, Afrika Kusini, Mauritania, na mwenyeji Côte d’Ivoire — wanaoshiriki kwenye mkutano wa siku mbili wa Africa CEO Forum 2025 ulioanza Jumatatu hii mjini Abidjan.
Mkutano huu umeandaliwa kwa ushirikiano na Shirika la Fedha la Kimataifa (IFC), ambalo ni sehemu ya kundi la Benki ya Dunia. Unawaleta pamoja zaidi ya viongozi 1,800 wa sekta binafsi barani Afrika pamoja na wawekezaji wa kimataifa kuanzia Mei 12 hadi 13, 2025.

Mkutano huu wa kila mwaka wa wakurugenzi wa sekta binafsi barani Afrika unakutanisha zaidi ya viongozi 2,000 wa biashara, wachumi, wawekezaji na watunga sera kutoka Afrika na ulimwenguni kote, kwa lengo la kuonyesha umuhimu wa sekta binafsi katika maendeleo ya bara la Afrika.
Misukosuko ya kiuchumi ya karibuni na mabadiliko ya vipaumbele vya misaada ya maendeleo duniani vimeleta wasiwasi kuhusu uwezo wa Afrika kufadhili maendeleo yake. Hii inaangazia sekta binafsi kama injini ya kweli ya maendeleo, kwa mujibu wa IFC.

Uwezo wa Afrika kujitegemea kiuchumi hapo baadaye utategemea usalama wa chakula, ubunifu wa kifedha, kasi ya teknolojia ya kidijitali na maendeleo ya viwanda — majukumu ambayo sekta binafsi inaweza kutekeleza kwa ufanisi.

Mkutano wa Africa CEO Forum 2025 huko Abidjan unafanyika kwa siku mbili ukihusisha mijadala ya juu, mazungumzo ya sera, mitandao ya kibiashara na warsha. Kauli mbiu ya mwaka huu ni: “Mikataba Mpya Kati ya Serikali na Sekta Binafsi: Afrika Inawezaje Kustawi Katika Uchumi Mpya wa Dunia?”
Lengo kuu ni kuimarisha ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi kwa ajili ya maendeleo endelevu ya bara la Afrika.


