Kundi la waasi wa M23 limemshukuru Rais Yoweri Kaguta Museveni wa Uganda, baada ya kuamua kufungua tena mipaka yote inayounganisha maeneo ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) yanayodhibitiwa na M23 na Uganda.
Mnamo Jumatano tarehe 9 Julai, Uganda ilitangaza uamuzi huo wa kufungua mipaka.
Tangazo hilo lilitolewa na Kanali Chris Magezi, kwa niaba ya Jenerali Muhoozi Kainerugaba, msemaji wa Jeshi la Ulinzi la Uganda (UPDF) na pia mwana wa Rais Museveni.
Magezi aliandika kwenye X (zamani Twitter) akisema kwa niaba ya Jenerali Muhoozi:
“Rais na Kamanda Mkuu wa UPDF ameagiza mipaka yote iliyo karibu na maeneo yanayodhibitiwa na M23 kufunguliwa mara moja. Hii inahusisha Bunagana, Ishasha, na maeneo mengine. Hakuna kitu kinachopaswa kuzuia biashara ya raia wetu.”
Akaongeza kuwa uchunguzi utafanyika ili kuwabaini viongozi waliohusika na kusimamisha biashara kati ya Wakongo na Waganda.
Asubuhi ya Alhamisi, tarehe 10 Julai, mipaka hiyo ilifunguliwa rasmi.
Kundi la M23, kupitia rais wake Bertrand Bisimwa, limetoa shukrani kwa Rais Museveni.
Aliandika kwenye X:
“Tunamshukuru Rais wa Jamhuri ya Uganda, Mheshimiwa Yoweri Museveni, kwa uamuzi wake wa kufungua tena mipaka yote ya mashariki mwa Congo. Huu ni uongozi unaojali watu na kuwaweka katika kiini cha maamuzi ya kisiasa.”
Mipaka hiyo, ikiwemo ya Bunagana, ilifungwa mnamo mwaka 2022, baada ya waasi wa M23 kuchukua udhibiti wa maeneo kadhaa, ikiwemo mji wa Bunagana.
Kwa mujibu wa Mamlaka ya Mapato ya Uganda, kufungwa kwa mipaka hiyo kulikuwa kunasababisha hasara ya zaidi ya shilingi milioni 500 kwa mwaka.


